0
WAZIRI wa Maji, Gerson Lwenge amesema watu wanaoiba miundombinu ya maji ni wahujumu uchumi wanaotakiwa kushitakiwa katika Mahakama ya Mafisadi.
Aidha, ametaka Shirika la Maji Safi na Maji Taka Dar es Salaam (Dawasco) kuhakikisha wanafikia wateja 400,000 kutokana na maji kuwapo ya kutosha.
Alisema hayo alipotembelea Maonesho ya 40 ya Biashara ya Kimataifa yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Nyerere, Barabara ya Kilwa, Dar es Salaam na kusema alipofanya ziara wilayani Mpwapwa, Dodoma alikutana na mtu ameiba mabomba 40.
Alisema mtu huyo kwa makusudi aliiba mabomba hayo na kufanya idadi kubwa ya watu kukosa. Alisema atachukuliwa adhabu kali kwani huo ni uhujumu uchumi.
Akizungumzia usambazaji wa maji katika mkoa wa Dar es Salaam alisema sasa wana wateja 250,000 lakini wafikie 400,000 Julai mwakani.
Akizungumzia upatikanaji wa maji, alisema miradi ya Ruvu Chini na Ruvu Juu imekamilika na inatoa maji kwa asilimia 100.

Post a Comment

 
Top