0
Rais wa Rwanda Paul Kagame amemtimua waziri wake wa afya Dr Agnes Binagwaho aliyeongoza wizara hiyo kwa kipindi cha miaka 5.
Dr Binagwaho alikuwa miongoni mwa mawaziri vigogo katika serikali ya Rwanda lakini wadadisi wanasema kutimuliwa kwake huenda kumetokana na utendaji kazi usioridhisha na matatizo yanayoikumba wizara hiyo kwa sasa.
Tangazo lililotiwa saini na waziri mkuu Anastase Murekezi limebainisha kuwa rais wa jamhuri katika mamlaka yake amemfuta kazi waziri huyo bila kutoa maelezo zaidi.
Lakini wadadisi wanasema huenda matatizo yaliyokuwa ndani ya wizara hiyo ndicho chanzo cha waziri huyo kutimuliwa.
Wakati wa mkutano wa kitaifa mwezi Desemba mwaka uliopita,waziri huyo alikosolewa vikali na washiriki waliobainisha tatizo kubwa la ugonjwa wa malaria.
Image captionDr Binagwaho alikuwa miongoni mwa mawaziri vigogo katika serikali ya Rwanda
Takwimu zilizopo kutoka wizara ya afya zilibainisha kuwa watu zaidi ya milioni 2.5 waliathirika na ugonjwa huo mwaka jana.
Hata hivyo katika kipindi cha miezi sita pekee ya mwaka huu wanahesabiwa wagonjwa milioni 1.,4 idadi ambayo ni kubwa sana ikilinganishwa na miaka 5 iliyopita ambapo Rwanda ilikuwa miongoni mwa mataifa yaliyokuwa katika nafasi nzuri ya kuangamiza ugonjwa huo.
Tatizo lililobainishwa na wakosoaji ni uzembe uliofanywa na wizara ya afya iliyoagiza vyandarua visivyotimiza viwango vya ubora na kugharimu wizara hiyo dolla milioni 15 za Marekani.
Katika ripoti ya mkaguzi mkuu wa mali ya umma,wizara ya afya ilibainisha pengo la milioni 10 dollar za Marekani zilizotoweka.
Kadhalika swala la utendajikazi mbovu wa hospitali za serikali linalotokana na madaktari bingwa wanaozikimbia hospitali hizo.
Image copyrightOTHER
Image captionwizara ya afya iliagiza vyandarua visivyotimiza viwango vya ubora na kugharimu wizara hiyo dolla milioni 15 za Marekani.
Mwezi uliopita waziri huyo alikiri kuwepo idadi kubwa ya madaktari wanaohamia katika hospitali binafsi wakikimbia mishahara midogo serikalini.
Kuna wanaoona kwamba maamzi yanayochukuliwa kuhusu hayaridhishi kukabiliana na matatizo hayo.
Kuhusu swala la malaria wizara ilikuwa na mkakati wa kutumia washauri wa afya ya uzazi katika kusaidia kutibu ugonjwa huo.
Aidha wizara ilikuwa na pendekezo kwamba waongezewe mshahara na kuruhusiwa kufanya kazi sehemu mbili.
Lakini mswada kuhusu hilo bado unajadiliwa bungeni.

Post a Comment

 
Top