0
Waziri mkuu wa Uingereza David Cameron, leo amefanya mkutano wake wa mwisho bungeni baada ya kuhudumu kwa miaka 6.
Kulishuhudiwa malumbano makali kati yake na kiongozi mkuu wa chama cha upinzani Labour, Jeremy Corbyn, kuhusiana na uchumi na migongano ya kungangania uongozi ndani ya vyama vyote vya kisiasa.
Leo ni siku ya mwisho kwa Bwana David Cameron kushikilia wadhifa wa waziri mkuu wa Uingereza, baada ya kuhudumu kwa miaka 6.
Akiwa bungeni Cameron amejibu maswali ya watunga sheria wa Uingereza na sasa anatarajiwa kukutana na Malkia Elizabeth katika ikulu ya Buckingham atakapowasilisha barua yake ya kujiuzulu rasmi.
Image copyrightAFP
Image captionAkiwa bungeni Cameron amejibu maswali ya watunga sheria wa Uingereza
Uchangamfu wa vikao vya bunge la Uingereza ulikuwepo kama kawaida lakini pia bw. Cameron alibadilishana mawazo kuhusu maswala muhimu ya kiuchumi na kiongozi wa chama kikuu cha upinzani cha Leba ,Bw Jeremy Corbyn.
Wakati huo kiongozi mpya wa chama cha Conservative Bi Theresa May alikuwa amekaa karibu naye.
Cameron alitangaza uamuzi wake wa kujiuzulu mwezi uliopita, baada ya kushindwa katika kura ya maoni kuhusu uanachama wa Uingereza katika muungano wa bara Ulaya EU.
Mrithi wake Bi May ameahidi kutekeleza uamuzi wa Uingereza kujiondoa kutoka muungano wa EU, licha ya yeye kupinga kauli kujiondoa.

Post a Comment

 
Top